Bi. Mary William akifurahia hati miliki ya eneo lake aliyoipata kupitia Kliniki ya Ardhi inayofanyika viwanja vya Community Centre, Halmashauri ya Mji Nzega, Mkoani Tabora, tarehe 16 Oktoba 2025.
Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Makazi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Deogratius Kalimenze akimkabidhi Bi. Constansia Kapama ambaye ni Mkazi wa Nzega Hati Miliki katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika viwanja vya Community Centre, Halmashauri ya Mji Nzega, Mkoani Tabora, tarehe 16 Oktoba 2025
Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Makazi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Deogratius Kalimenze akimkabidhi Bi. Odilia Golagoza ambaye ni Mkazi wa Nzega Hati Miliki katika Kliniki ya Ardhi inayofanyika viwanja vya Community Centre, Halmashauri ya Mji Nzega, Mkoani Tabora, tarehe 16 Oktoba 2025.
………..
Wanawake katika Halmashauri ya Mji Nzega mkoani Tabora wameanza kunufaika na azma ya serikali kuhakikisha wanamiliki ardhi kama ilivyoainishwa katika sera ya ardhi ya mwaka 1995 toleo la mwaka 2023.
Katika siku ya pili ya Kliniki ya Ardhi inayoendela katika viwanja vya Community Centre, wanawake waliokuwa wakifuatilia hati miliki za ardhi katika kliniki hiyo wamepatiwa hati zao na Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Makazi Bw. Deogratius Kalimenze.
‘‘Sera ya Ardhi ya mwaka 1995 toleo la mwaka 2023 limeweka msukumo mkubwa katika kuhakikisha usawa wa kijinsia, kwa kutambua haki za wanawake kumiliki na kurithi ardhi, pamoja na kushirikishwa kikamilifu katika maamuzi ya matumizi ya ardhi katika familia na jamii’’ amesema Kalimenze.
Miongoni mwa wanawake waliopata hati miliki Bi. Constansia Kapama alieleza furaha yake baada ya kupokea hati miliki ya kiwanja chake, akisema hatua hiyo imempa uhakika wa umiliki na uwezo wa kutumia ardhi yake kama rasilimali ya maendeleo.
“Tunaishukuru sana Serikali kwa kutuletea huduma hii ya ardhi karibu nyumbani imeturahisishia sana, naomba niwahamasishe na wanawake wenzangu wafike kwa wingi kufuatilia hati zao’’ amesema Bi. Constansia.
Nae Bi. Odilia Golagoza ambaye amepokea hati miliki mbili za maeneo yake aliishukuru Serikali kwa kuwawezesha wanawake kumiliki ardhi na kusema kuwa yuko tayari kuhamasisha wanawake wa Sagara wafuatilie hati zao ili waweze kuwa na umiliki wa maeneo yao.
Kwa upande wake, Kamishna wa Ardhi Msaidizi Mkoa wa Tabora Bw. Tumaini Gwakisa amesema kuwa, Kliniki ya Ardhi ni sehemu ya jitihada za Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi za kusogeza huduma karibu na wananchi, huku ikizingatia usawa wa kijinsia katika umiliki wa ardhi kwa njia ya utoaji elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa wanawake kumiliki ardhi na umiliki wa ardhi wa pamoja kati ya mume na mke.
Kliniki ya Ardhi katika Halmashauri ya Mji Nzega imeanza tarehe 15 Oktoba 2025 na itahitimishwa tarehe 24 Oktoba 2025 ikiwa na lengo la kutoa huduma za ardhi kama Utoaji wa hati miliki za ardhi papo kwa papo, Utatuzi wa migogoro ya ardhi, Makadirio ya kodi ya pango la ardhi, Uhuishaji milki zilizoisha muda wake pamoja na kutoa Elimu na ushauri kuhusu masuala ya ardhi.