NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) kimeboresha kwa kiwango kikubwa miundombinu yake ya TEHAMA kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Uchumi (HEET), hatua itakayoongeza ufanisi katika ufundishaji, ujifunzaji na utoaji wa huduma za kimtandao chuoni hapo.
Akizungumza mbele ya wahariri wa vyombo vya habari waliotembelea chuo hicho leo Oktoba 21, 2025 kuona maendeleo ya utekelezaji wa mradi, Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. William Anangisye, amesema UDSM sasa ina uwezo wa kupokea na kusambaza mtandao wa 10Mbps kutoka uwezo wa awali wa 1.5Mbps, jambo litakalorahisisha upatikanaji wa taarifa na maudhui ya masomo kwa njia ya kidijitali.
Aidha, kumbi za mihadhara zenye uwezo wa kuchukua jumla ya wanafunzi 8,000 kwa wakati mmoja zimewekewa vifaa vya kisasa vya kufundishia, ikiwa ni sehemu ya maboresho ya mazingira ya kusomea.
“Kwa sasa wanafunzi 39,000 wakiwemo 165 wenye mahitaji maalum pamoja na walimu 600 wameshaingizwa kwenye mfumo huu,” amesema Prof. Anangisye .
Kuhusu maboresho ya taaluma, Prof. Anangisye amesema jumla ya mitaala 250 imefanyiwa mapitio ili kuendana na mahitaji ya soko la ajira na uchumi wa kisasa.
“Mitaala hii imeandaliwa kwa kuzingatia ushauri wa wadau, hususan waajiri. Tumeongeza msisitizo kwenye mafunzo kwa vitendo ili mhitimu wa UDSM awe na maarifa, ujuzi na amali kulingana na Dira ya Maendeleo ya Taifa 2050,” ameongeza.