Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo ambaye ameelezea umuhimu wa mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa makundi ya wajasiriamali wadogo huku akiitaka OSHA kuhakikisha mafunzo hayo yanakuwa endelevu.
Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, akitoa maelezo ya awali kuhusu mafunnzo ya usalama na afya kazini yalitolewa na OSHA kwa wanawake wanaojihusisha na uzalishaji wa bidhaa za batiki Dar es Salaam
Na. Fredy Mgunda
Wanawake zaidi ya 200 wanaojihusisha na utengenezaji bidhaa za batiki wamenufaika na mafunzo ya usalama na afya yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kufanya shughuli zao za kila siku kwa kuzingatia kanuni bora za usalama na afya mahali pa kazi.
Mafunzo hayo ya siku moja yaliyogharamiwa na serikali yametolewa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) katika eneo la Ilala Jijini Dar es Salaam ambapo mada mbalimbali zikiwemo dhana ya usalama na afya mahali pa kazi, vihatarishi vya usalama na afya katika shughuli za uzalishaji bidhaa za batiki pamoja huduma ya kwanza mahali pa kazi zimefundishwa.
Mafunzo hayo yamefunguliwa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Mhe. Rahma Kisuo ambaye ameelezea umuhimu wa mafunzo ya usalama na afya mahali pa kazi kwa makundi ya wajasiriamali wadogo huku akiitaka OSHA kuhakikisha mafunzo hayo yanakuwa endelevu.
“Wajasiriamali wadogo ni kundi muhimu sana na lenye mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa Taifa letu hivyo ni muhimu kuwapatia mafunzo ili waweze kutekeleza shughuli zao katika hali ya usalama,” amesema Naibu Waziri.
Aidha, amesisitiza kuwa mafunzo hayo yatasaidia kupunguza ajali, magonjwa na vifo vinavyoweza kutokea kutokana ukosefu wa mifumo ya usalama na afya ikiwemo wafanyakazi wenye uelewa wa masuala husika.
Sambamba na hayo, ametoa wito kwa wafanyabiashara hao kutojihusisha na makundi yenye nia ya kuvuruga shughuli za uzalishaji na kuvunja amani ya nchi ya Tanzania.
Awali, Mtendaji Mkuu wa OSHA, Bi. Khadija Mwenda, amesema mafunzo hayo ni mwendelezo wa utekelezaji wa program atamizi ya wajasiriamali wadogo ya Taasisi hiyo ijulikanayo- Afya Yangu, Mtaji Wangu.
“OSHA ilibuni na kutekeleza program ya Afya Yangu-Mtaji Wangu ili kuziba mwanya wa uelewa wa masuala ya usalama na afya uliopo baina ya sekta rasmi na sekta isiyo rasmi hivyo kupitia program hii tumekuwa tukiainisha makundi mbalimbali ya wajasiriamali wadogo na kuyawezesha kwa mafunzo pamoja na kuwapatia vifaa kinga muhimu kutegemeana na aina ya shughuli zao,” amesema Mtendaji Mkuu wa OSHA.
Aidha, amesema program hiyo itaendelea kutolewa kwa makundi mbalimbali hususan vijana ambao kwa mujibu wa tafiti za OSHA za hivi karibuni ndio waathirika wakubwa wa ajali katika maeneo ya uzalishaji kutokana na uelewa mdogo na ukosefu wa uzoefu kazini.
Akitoa maoni yake katika mafunzo hayo, mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Jesca Charles, ameishukuru OSHA kwa kuwapatia elimu na vifaa kinga ambavyo vitawasaidia kujikinga dhidi ya vihatarishi vya ajali na magonjwa hususan kemikali ambacho ndio kihatarishi kikubwa katika uzalishaji wa bidhaa za batiki.







