
Mgodi wa Barrick Buzwagi ambao uko katika mchakato wa kufungwa umefadhili mradi wa ujenzi wa chujio la maji ya mvua eneo la Mwendakulima wilayani Kahama mkoani Shinyanga unaogharimu takribani shilingi Bilioni 4.8 kwa ajili ya kuwapatia wananchi wa mji wa Kahama maji safi na salama.
Akiongea wakati wa hafla ya kupokea mwenge ulioambatana na kuweka jiwe la msingi la ujenzi huo wa mradi wa maji, Meneja wa Ufungaji wa Mgodi wa Buzwagi ,Zonnastraal Mumbi amesema mgodi katika hatua zake za mwisho za ufungaji umeamua kufadhili mradi huo ili kuondoa tatizo la upatikanaji wa maji kwenye Wilaya ya Kahama.
“Haya ni matokeo ya ufungaji wa mgodi wa Buzwagi kwa kuamua kufadhili mradi mkubwa kabisa wa maji ya mvua kwa kutengeneza miundombinu ya uvunaji , ukusanyaji na usambazaji wa maji ya mvua kwa ajili ya matumizi wa wananchi wa mji ya Kahama,” amesema Mumbi.
Ameongeza kuwa, moja ya dhamira ya kampuni ya Barrick inayoendeha shughuli zake nchini kwa ubia na Serikali kupitia kampuni ya Twiga Minerals ni kuunga mkono jitihada za Serikali kuhakikisha wananchi wanapata maji safi na salama.
“Mgodi wa Buzwagi umefadhili mradi huu wa maji ya mvua kwa 62% kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miundombinu ya kisasa na bora inajengwa kwenye mradi huu kama sehemu za kuleta matokeo chanya kwa wananchi wa mji wa Kahama,” amesema.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Usambazaji Maji na Usimamizi wa Mazingira, Mamlaka ya Maji Safi wa Mazingira Kahama (KUWASA), Mhandisi , Magige Marwa , ametoa pongezi kwa kampuni ya Barrick nchini kwa kufadhili mradi huo mkubwa ambao ukikamilika utaondoa changamoto ya upatikanaji maji safi na salama wilayani Kahama.
Ameongeza kwamba mradi wa ujenzi wa chujio la maji Mwendakulima unatazamiwa kuhudumia zaidi ya 66% ya wakazi waishio Manispaa ya Kahama na una uwezo wa kuzalisha lita milioni 10 kwa siku.
“Mradi huu unatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu na mpaka sasa 78% ya mradi mzima umeshakamilika kutokana na kasi ya ujenzi wa mradi huu mkubwa kwenye mji huu wa Kahama,” amesema.
Mhandisi Marwa amefafanua kwamba mradi huo wa chujio la maji ya mvua 62% imefadhiliwa na mgodi wa Barrick- Buzwagi na 38% ni KUWASA kupitia Wizara ya Maji na Serikali ya Jamhuri wa Muungano wa Tanzania.
Kwa upande wake , Kiongozi wa mbio za mwenge wa Uhuru , Ismail Ali Ussi amesema Wizara ya Maji inaendelea kufanya vizuri na kutekeleza kwa vitendo maono ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kumtua mama ndoo kichwani kwa kupeleka huduma ya maji mijini na vijijini.
“Nachukua fursa hii kuwapongeza wataalamu wote wa Wizara na mamlaka za maji hapa kahama kwa kufanya kazi usiku na mchana katika kuhakikisha watanzania wanapata maji safi na salama,” amesema.
Naye, Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Frank Nkinda amesisitiza kwamba umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii na kuendelea na ari hiyo ya kutekeleza miradi ya huduma za wananchi kwa viwango vya juu ili kukidhi mahitaji ya wananchi.