Na Linda Akyoo -Moshi
Watu watatu wamefariki dunia papo hapo baada ya gari dogo aina ya Toyota Rav4 kugongana uso kwa uso na basi la abiria la Kampuni ya Ester Luxury, katika eneo la Mdawi, Wilaya ya Moshi, mkoani Kilimanjaro, leo Jumamosi, Februari 1, 2025.
Akizungumza na waandishi wa Habari,Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji mkoani Kilimanjaro, Jeremiah Mkomagi, amkiri kutokea Kwa ajali iyo na kusema kuwa ajali hiyo imetokea asubuhi baada ya dereva wa Toyota Rav4 kupita magari mengine bila kuchukua tahadhari, hali iliyopelekea kugongana uso kwa uso na basi lililokuwa likitokea Moshi kwenda Dar es Salaam.
Aidha Mkuu wa Wilaya ya Moshi Mhe.Godfrey Mzava amesema kuwa hakuna majeruhi kwenye basi hilo, lakini watu watatu waliokuwa kwenye gari dogo wamepoteza maisha papo hapo.
Miili ya marehemu wakiwemo wanaume wawili na mwanamke mmoja imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro, Mawenzi, huku mamlaka zikihimiza madereva kuwa waangalifu barabarani ili kuepusha ajali kama hii.