Maadhimisho hayo yaliyobeba kaulimbiu ya “Haki na Maisha Endelevu kwa Mlaji” yamelenga kutoa elimu kwa wadau na wananchi katika kuongeza juhudi za walaji kujisimamia, kuzingatia haki na wajibu wao katika soko.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 7, 2025 Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani nchini (FCC) William Erio, amesema maadhimisho hayo yamelenga pia kuwakumbusha wafanyabiashara kuzingatia haki za mlaji wanaposambaza bidhaa na huduma sokoni.
“FCC tulianza kufanya maadhimisho ya siku hii tangu mwaka 2009 na tumeendelea kufanya hivyo kwa kutoa elimu kwa Umma na wadau mbalimbali nchini kwa kushirikiana na vyombo vingine vya Kumlinda Mlaji” amesema Erio.
Kwa upande wake, Meneja Miradi wa Shirika la Foundation for Civil Society (FCS) Charles Kainkwa amesema, wamejitokeza kuunga mkono juhudi za FCC katika kutoa elimu na hamasa ya kutambua haki na wajibu kwa walajii na wadau wa bidhaa mbalimbali nchini, ikiwa ni sehemu ya wajibu wao kuwa mstari wa mbele kutoa uelewa na mwamko kwa wananchi kuhusu masuala mbalumbali ya jamii na kitaifa kwa ujumla.
Amesema kuwa Ushirikiano huo unaonesha umuhimu wa walaji kufahamu haki zao na njia zilizopo za kuripoti malalamiko yao, nakwamba ulinzi wa walaji ni muhimu katika kulinda masoko yenye nguvu.“Ulinzi wa walaji ni muhimu katika kulinda masoko yenye nguvu na ufanisi, hali inayochochea maendeleo ya biashara na sekta ya uchumi kwa ujumla. Wakati wafanyabiashara wanapoheshimu haki za walaji, na walaji wanapozielewa haki zao, mazingira mazuri ya kibiashara na kijamii huimarika.
“FCS Kama mdau wa maendeleo, inaendelea kujitolea kuimarisha haki za kijamii na kiuchumi, na kuinua kiwango cha maisha nchini Tanzania” amesema KainkwaSiku ya Haki za Mlaji Duniani ambayo hufanyika Machi 15 kila mwaka, iliasisiwa na aliyekuwa Rais wa Marekani, John F. Kennedy, Machi 15, mwaka 1962 katika Bunge la Congress, kubainisha haki za awali za Mlaji ambazo zilisababisha utambuzi wa Haki Nane za Mlaji zinazotambuliwa katika Mataifa yote duniani.