Na Mwandishi wetu, Mirerani
MAMIA ya wakazi wa Wilaya ya Simanjiro Mkoani Manyara, wameshiriki Iftari iliyoandaliwa na DC Simanjiro Fakii Raphael Lulandala na kufanyika Mji mdogo wa Mirerani.
Iftari hiyo imehusisha watoto yatima, wenye kuishi kwenye mazingira magumu, wajane, viongozi wa madhehebu ya dini, wazee maarufu, wadau wa madini, wakuu wa taasisi na viongozi mbalimbali.
Katika Iftari hiyo, watoto yatima, wenye uhitaji na wajane wamepatiwa mbuzi wawili, kondoo mmoja, mchele kilo 50, sukari kilo 50, mafuta lita 20, maji katoni tano na sharubati katoni tatu, ili kusherehekea sikukuu ya iddi.
Pia, katika Iftar hiyo viongozi wa dini na watu waliohudhuria walifanya dua ya kumuombea afya njema, hekima na amani, Rais Samia Suluhu Hassan, DC Lulandala, viongozi wa Serikali na wananchi kwa ujumla katika kujenga Taifa la maendeleo na amani.
DC Lulandala akizungumza kwenye Iftari hiyo amewashukuru viongozi na watu wote wa madhehebu mbalimbali waliohudhuria Iftar hiyo.
“Nilivyoingia ukumbini na kukuta hali ilivyo kidogo nitoe machozi kwa furaha kwani watu wa madhehebu tofauti wamekaa kwenye meza wakifurahia kwa pamoja,” amesema DC Lulandala.
Pia, amewahakikishia kuwa uchaguzi mkuu utafanyika mwaka huu, kama ilivyopangwa na viongozi wa dini kuwaombea pia baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa watangulize maslahi ya jamii kuliko maslahi yao na wawe na akili timamu kila wanapozungumza.
Katibu Tawala wa wilaya ya Simanjiro (DAS) Warda Abeid Maulid amesema jamii inapaswa kujikinga na maambukizi ya homa ya nyani (Mpox) kwa kutumia mtindo wa maisha ilivyokuwa Covid 19 kwa kunawa mikono kila mara.
Sheikh wa wilaya ya Simanjiro, Ramia Isanga amempongeza DC Lulandala kwa kuandaa Iftar hiyo ambayo imewahusisha jamii ya madhehebu mbalimbali.
“Kwa kweli hapa umepanda mbegu bora ya upendo, umoja na mshikamano kwenye mioyo ya watu na ninatarajia kupitia hili tutaendelea kuwa na amani bila kubaguana na kufanikisha maendeleo,” amesema Sheikh Isanga.
Paroko msaidizi wa Kanisa Katoliki Parokia ya Bikira Maria Malkia wa Rozali Takatifu, Padri Krisantus Asenga amesema jambo hilo ni jema kwani limewakuta hata wakristo wanafunga kwaresma.
Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Simanjiro Kiria Ormemei Laizer amesema kitendo cha jamii na viongozi kushiriki Iftar kwa pamoja kupitia DC Lulandala ni ya kupongezwa mno.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Baraka Kanunga amempongeza DC Lulandala kwa kuandaa Iftar hiyo ambayo imewaweka pamoja watu wa madhehebu tofauti.
Wadau wa maendeleo Lengai Ole Makoo na Taiko Ole Kulunju wamempongeza DC Lulandala kwa kuandaa Iftar hiyo iliyoleta jamii na viongozi kwa ukaribu na pamoja.