Serikali imeendelea kusisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi wa taasisi zake za kibiashara kwa kuzingatia ushindani wa sekta binafsi, huku ikieleza haja ya kuimarisha ushiriki wa kampuni ambazo ina umiliki wa hisa chache ili ziwe na mchango mkubwa zaidi katika maendeleo ya uchumi wa taifa.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, akifungua Mkutano wa Wakurugenzi wa Bodi za Kampuni ambazo Serikali ina Umiliki wa Hisa Chache, ulioanza Jumatano Machi 26, 2025, katika Shule ya Uongozi ya Mwalimu Nyerere wilayani Kibaha, amesema:
“Nafanya mahesabu hapa, naona kuwa mchango wa taasisi 17 unazidi hata ule wa taasisi ambazo serikali inamiliki kwa wingi. Swali nililouliza mwaka jana na nalirudia tena mwaka huu ni, ni kitu gani mnachofanya ambacho sisi serikalini hatufanyi? Kama mnaweza kufanya vizuri kiasi hiki, kwanini taasisi zote za serikali zisiwe kama ninyi? Hii inamaanisha kwamba kama serikali, tunapaswa kuachia umiliki wa taasisi hizi haraka ili ziweze kufanya vizuri zaidi.”
Waziri Mkumbo amesisitiza kuwa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inalenga kuwa na uchumi unaoendeshwa na sekta binafsi yenye ushindani wa kitaifa na kimataifa.
“Hivi sasa tunakamilisha maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, na dhamira yetu ni kuwa na malengo makubwa zaidi kuliko tuliyonayo sasa. Katika dira hii, sekta binafsi itakuwa mhimili mkuu wa uchumi, si tu ndani ya nchi bali hata kimataifa. Tunapaswa kupanua biashara zetu nje ya Tanzania na hata nje ya bara la Afrika.”
Amewataka viongozi wa kampuni hizo kujiwekea mikakati ya muda mrefu kwa maendeleo ya taasisi zao na kuzitaka taasisi hizo kujiwekea eneo lao la kimkakati ambalo litaifanya taasisi kuwa bora na shindani zaidi duniani, akitolea mfano Rais Samia Suluhu Hassan alivyoweka malengo makubwa kwa Tanzania kuwa kinara wa uzalishaji wa kilimo Afrika na kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa chakula duniani ifikapo 2050.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais Mipango na Uwekezaji, Dkt. Tausi Kida, akizungumza katika mkutano huo, ameeleza kuwa maandalizi ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yanazingatia kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na Biashara