Na Mwandishi Wetu-Dodoma
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kuhamasisha watanzania kuwa na desturi ya kujenga miundombinu na kuvuna maji ya mvua kwa kila msimu wa mvua ili kuwa na uhakika wa maji kwa kipindi cha mwaka mzima hususani kipindi cha kiangazi.
Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Dkt James Andilie amesema hamasa hiyo inalenga kuwafanya wananchi kuona umuhimu wa kuvuna maji ya mvua ambayo yanaweza kutumiwa kumwagilia mimea, kunywesha wanyama na watu.
“Uvunaji wa maji ya mvua ni mbinu ambayo inazuia maji ya mvua kutiririka hovyo, badala yake tunaweza kuyakusanya na kuyahifadhi kwa matumizi mbalimbali”. Alisisitiza.
EWURA hudhibiti mamlaka za majisafi na usafi wa mazingira nchini ambapo moja ya jukumu lake ni kuhakikisha zinaimarisha hali ya uzalishaji na usambazaji wa maji nchini ikiwa ni pamoja kusimamia utekelezaji wa mikakati na miongozo mbalimbali ya kuboresha huduma .
Vilevile, Dk. Andilile amesisitiza kuwa, uvunaji wa maji ya mvua unaweza kuleta uhakika wa maji na kuwa chanzo mbadala cha maji kwa mamlaka. EWURA ilianza kuhamasisha uvunaji maji ya mvua Mei, 2023.