Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limeendelea kutoa elimu kuhusu masuala ya viwango kwa wananchi na wajasiriamali katika Maonesho ya 12 ya Biashara na Utalii yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mwahako City Garden, mkoani Tanga.
Akizungumza katika maonesho hayo, Afisa Udhibiti Ubora wa TBS, Bw. Abdul Ngozoma, ametoa wito kwa wajasiriamali kujitokeza kwa wingi kuthibitisha ubora wa bidhaa zao kupitia Shirika hilo.
Amesema kuwa kuthibitisha ubora wa bidhaa si tu ni hatua ya kuongeza ushindani wa bidhaa sokoni, bali pia inalenga kulinda afya ya walaji.
Aidha, Bw. Ngozoma ameongeza kuwa huduma hiyo hutolewa bila malipo kwa wajasiriamali wadogo, ikiwa ni sehemu ya juhudi za TBS kuwawezesha na kuwainua kiuchumi.