Benki ya Access Tanzania yapanua huduma zake nchini, yaimarisha huduma za kibinafsi na biashara, na kuchochea ujumuishaji wa kifedha kwa Watanzania wote.
Dar es Salaam, 23 Juni 2025 – Access Bank Tanzania leo imetangaza rasmi kukamilika kwa mafanikio ya ununuzi wa kitengo cha Huduma za Wateja wa Kawaida, Binafsi na Biashara cha Benki ya Standard Chartered Tanzania, baada ya kukamilika kwa taratibu zote muhimu za kisheria na kupokelewa kwa idhini kutoka kwa mamlaka husika za udhibiti.
Hatua hii inaashiria mafanikio makubwa katika safari ya mageuzi ya Access Bank Tanzania kama benki ya biashara kamili inayolenga utoaji wa huduma jumuishi, salama, na za kidijitali kwa watu binafsi, wajasiriamali, na wafanyabiashara nchini kote.
“Ununuzi huu hauhusiani tu na upanuzi wa huduma bali ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi yetu ya kuwafikia Watanzania wengi zaidi kwa huduma za kibenki za kiwango cha kimataifa zinazoweka mteja mbele,” alisema Imani John, Mkurugenzi Mtendaji wa Access Bank Tanzania.
“Kwa kuchanganya uzoefu wa Standard Chartered katika huduma za kifedha na mtazamo wa kidijitali unaoongozwa na Access Bank pamoja na mtandao wetu barani Afrika, tunajenga jukwaa madhubuti la uwezeshaji wa kifedha kwa wote.”
Kupitia ununuzi huu, Access Bank Tanzania imeongeza kwa kiasi kikubwa uwezo wake wa kuwahudumia Watanzania, na kuchangia kwa dhati ajenda ya taifa ya ujumuishaji wa kifedha. Benki sasa itaweza kutoa huduma zilizobuniwa mahsusi kulingana na mahitaji ya makundi mbalimbali ya jamii, yakiwemo watu wasiokuwa na akaunti benki, wenye kipato kikubwa, wamiliki wa biashara ndogo na za kati Akaunti za Biashara, wanawake na vijana.
