Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mha. Hamad Yusuph Masauni (Mb) amewataka Watanzania kutochukulia poa suala la Utunzaji wa Mazingira badala yake kuyatunza Mazingira ili yaendelee kuwa sehemu salama ya kuishi.
Mhe. Masauni ameyasema hayo leo tarehe 25 Juni, 2025 alipokuwa akizungumza na Menejimenti ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kwenye Kikao Kazi kilichofanyika jijini Dodoma kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi za Baraza.
Mhe. Masauni amesema katika kuhakikisha suala la Utunzaji wa Mazingira linakuwa endelevu Baraza linatakiwa kuwekeza nguvu zaidi katika eneo la utoaji wa huduma na elimu kwa Umma ili Watanzania waielewe Sheria ya Usimamizi wa Mazingira na kuona wana wajibu wa kuyatunza Mazingira.
Amesema Baraza lina jukumu kubwa la kuhakikisha Mazingira yanatunzwa na ili suala hilo lifanikiwe ni lazima kila mmoja wetu kutimiza majukumu yake katika uhifadhi na Usimamizi wa Mazingira.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa Baraza Dkt. Immaculate Sware Semesi amempongeza Waziri kwa kutoa nafasi ya kujumuika na Menejimenti ya Baraza na kupokea maoni mbalimbali yaliyotolewa kwa ustawi wa Baraza na Taifa kwa ujumla.