Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai, wameonya juu ya mwenendo hatarishi duniani wa kupunguza au kupuuza bajeti za elimu hasa wakati wa misukosuko ya kiuchumi na kisiasa.
Wakizungumza kwenye mjdala kuhusu elimu uliofanyika Jumapoili usiku katika hoteli ya Johari Rotana jijini Dar es Salaam, viongozi hao wawili waliwataka viongozi wa serikali, wafadhili na washirika wa maendeleo kulinda na kuendeleza uwekezaji kwenye elimu, wakisisitiza kuwa elimu ndiyo msingi wa maendeleo ya kudumu.
“Elimu haipaswi kuwa mhanga wa kwanza wakati wa janga. Si anasa—ni uhai wa maendeleo,” alisema Dkt. Kikwete. “Tukiacha kuwekeza katika elimu leo, tunajitengenezea matatizo makubwa kesho.”
Malala aliongeza kuwa madhara ya kupunguzwa kwa bajeti ya elimu huathiri zaidi wasichana. “Kila matatizo yanapotokea, wasichana ndiyo huathirika kwanza—hutolewa shule, ndoto zao hukatizwa. Hili si tu dhuluma, bali ni upumbavu wa kisera,” alisema.
Katika ziara yao katika Shule ya Sekondari Kibasila siku ya Jumatatu, Dkt. Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Bodi ya GPE, alitangaza kuwa Tanzania itapokea msaada wa dola milioni 88 za Kimarekani kuanzia mwakani.
Dkt. Kikwete alisema tangu kujiunga na GPE mwaka 2013, Tanzania imepokea zaidi ya dola milioni 344 zilizowezesha ujenzi wa zaidi ya madarasa 3,000, vyoo 7,600, nyumba za walimu 64, shule mpya 18, vituo vya walimu 252, na usambazaji wa vitabu milioni 36.
Kwa upande wake, Malala alitangaza msaada wa dola milioni 3 kutoka kwenye Malala Fund kusaidia wasichana waliokatishwa masomo kutokana na ujauzito au sababu nyingine za kijamii.
Malala pia alipongeza hatua ya serikali ya Tanzania ya mwaka 2021 ya kuruhusu wasichana waliopata ujauzito kurejea shule.
“Uamuzi huu ulikuwa wa kishujaa na wa kibinadamu,” alisema. “Wasichana sasa wanaweza kurudi shule ndani ya miaka miwili au kujiunga na vituo vya elimu mbadala.”
Hata hivyo, wote walikiri changamoto bado zipo, na kwamba chini ya asilimia 50 ya wasichana wanaokamilisha shule ya msingi, na ni asilimia 16 pekee wanaoendelea hadi sekondari ya juu, sababu kubwa zikiwa ni umaskini, mila kandamizi, na uhaba wa miundombinu.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga, alieleza kuwa kupitia Mpango wa Samia Scholarship ulioanzishwa 2023, wasichana 1,320 tayari wamenufaika kwa kusomea kozi za sayansi vyuo vikuu.
“Mpango huu pamoja na sera ya re-entry ni silaha muhimu kuhakikisha wasichana hawapotei kwenye mfumo wa elimu,” alisema.

Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa na Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu.
Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai akivishwa skafu alipowasili kutembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu.
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika moja ya madarasa walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu.
Mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai akiwa na baadhi ya wanafunzi wanamichezo alipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaamsiku ya Jumatatu.
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakimwagilia mti baada ya Malala Kuupanda, walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu. Kushoto ni Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mh. Omary Kipanga
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakati yeye na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai walipotembelea shule ya sekondari ya Kibasila wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam siku ya Jumatatu.
Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete na mwanaharakati wa elimu wa kimataifa na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Malala Yousafzai wakiwa katika mazungumzo ofisini kwa Rais Mstaafu siku ya Jumatatu