

Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza ratiba ya kuchukua fomu za uteuzi kwa wagombea wa vyama 14 vya siasa waliopendekezwa kugombea nafasi za Kiti cha Rais na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inaanza leo tarehe 09 Agosti, 2025.
Mkurugenzi wa INEC, Ndugu, Kailima R. K akizungumza jijini Dodoma Agosti 8, 2025 amewataja wagombea watakaochukua fomu kesho tarehe 09 Agosti, 2025 kuwa ni kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM), National Reconstruction Alliance (NRA) na Alliance for African Farmers Party (AAFP).
“Hadi leo tarehe 08 Agosti, 2025, tumepokea barua kutoka katika vyama vya siasa kumi na nne (14) zikiainisha tarehe na muda ambao wanachama wa vyama vyao waliowapendekeza kugombea nafasi za Kiti cha Rais na Makamu wa Rais watafika ofisi za Tume zilizopo Njedengwa Jijini Dodoma kwa ajili ya kuchukua Fomu za Uteuzi,” amesema Ndugu. Kailima.
Amevitaja vyama vingine na tarehe za wagombea kuchukua fomu kuwa ni pamoja na na Chama cha MAKINI tarehe 10 Agosti, 2025, The National League for Democracy (NLD) tarehe 10 Agosti, 2025, United Peoples’ Democratic Party (UPDP) tarehe 10 Agosti, 2025 na African Democratic Alliance Party (ADA – TADEA) tarehe 11 Agosti, 2025.
Vyama vingine ni Union for Multiparty Democracy (UMD) tarehe 11 Agosti, 2025, Tanzania Labour Party (TLP) tarehe 11 Agosti, 2025, Chama Cha Kijamii (CCK), tarehe 12 Agosti, 2025, Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), tarehe 12 Agosti, 2025, Alliance for Democratic Change (ADC), tarehe 12 Agosti, 2025, Democratic Party (DP) tarehe 13 Agosti, 2025 na National Convention for Construction and Reform (NCCR – MAGEUZI) tarehe 15 Agosti, 2025.
Ndugu Kailima amesema tayari Tume imeviandikia vyama hivyo vya siasa barua kuvijulisha kuhusu ratiba hiyo ya utoaji fomu za uteuzi.
“Aidha, ni muhimu tukumbuke kuwa, ratiba hii inahusu vyama kumi na nne (14) pekee vilivyowasilisha taarifa hadi kufikia leo tarehe 08 Agosti, 2025, hivyo iwapo vyama vingine vitajitokeza, tutaandaa ratiba husika na kuwajulisha,” amesema.
Amevipongeza vyama vyote vya siasa kwa kuendelea kufanya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025.