FARIDA MANGUBE,MOROGORO
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeibuka Mshindi wa Jumla na Mshindi wa Kwanza kwa upande wa Taasisi za Mafunzo na Utafiti katika kilele cha Maadhimisho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Mwalimu J.K. Nyerere, Morogoro mwaka 2025.
Katika mashindano hayo, SUA pia kupitia Ndaki ya Kampasi ya Mizengo Pinda kimepata ushindi wa pili kwa upande wa Taasisi za Elimu katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, yaliyofanyika kwenye Viwanja vya John Mwakangale, Mbeya.
Akizungumzia ushindi huo, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu SUA, Profesa Raphael Chibunda, alisema mafanikio hayo yametokana na mshikamano wa wafanyakazi, wanafunzi na wadau mbalimbali katika kuandaa na kuwasilisha ubunifu, teknolojia na tafiti zenye mchango mkubwa katika maendeleo ya kilimo nchini.
“Tunawapongeza na kuwashukuru wote waliotoa mchango wao kufanikisha ushindi huu, na tunahimiza kuendelezwa kwa ari, mshikamano na ubunifu ili kufanikisha mafanikio makubwa zaidi katika siku zijazo,” alisema Profesa Chibunda.