Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Benki ya NMB imedhamini na kushiriki kikamilifu Kongamano la Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) 2025, lililofanyika Agosti 13 jijini Dodoma, likiwa na lengo la kutathmini na kuenzi mchango wa mashirika hayo katika maendeleo ya Taifa kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita.
Kongamano hilo limehitimishwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, akimuwakilisha Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Isidory Mpango, ambaye amesisitiza jukumu la Serikali kuboresha mazingira ya utendaji wa NGOs ili yaendelee kushirikiana na Serikali katika sekta muhimu ikiwemo afya, kilimo, elimu, maji, mazingira, utawala bora, mifugo na uvuvi.
Kupitia banda lake, NMB imewasilisha masuluhisho ya kifedha yanayolenga kuimarisha mashirikiano na mashirika yasiyo ya kiserikali nchini, sambamba na mchango wake katika kukuza sekta ya fedha na kusaidia utekelezaji wa miradi ya kijamii.
Uwakilishi wa benki hiyo umeongozwa na Mkuu wa Idara ya Biashara ya Serikali, Bi. Vicky Bishubo, akiambatana na viongozi wengine wa NMB, ambao wametoa ufafanuzi wa huduma na bidhaa zinazoweza kusaidia NGOs kuongeza ufanisi na uendelevu wa shughuli zao.
Kwa udhamini huu, NMB imeendelea kudhihirisha dhamira yake ya kushirikiana na wadau mbalimbali kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukuza maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.