Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania Jenerali Jacob John Mkunda leo tarehe 12 Septemba 2025 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Shule ya Polisi Jeshi katika kijiji cha Mkanzaule Wilaya ya Mafinga Mkoani Iringa.
Akizungumza wakati wa sherehe hizo, Jenerali Mkunda alisema kuwa kwa upande wa Jeshi ni historia na ni mara ya kwanza kwa Polisi Jeshi kuwa na shule yao ya kujitegemea huku akimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuunga mkono uboreshaji wa miundo mbinu ya mafunzo jeshini.
Pia alisema uamuzi wa kujenga shule hiyo ni jawabu mojawapo la kuhakikisha Polisi Jeshi wanapata mafunzo yenye utaalamu wa kuwawezesha kutekeleza majukumu yao ya kipolisi kwa weledi mkubwa na ufanisi mkubwa.
Aidha, akizungumza mara baada ya uwekaji wa jiwe la msingi, Jenerali Mkunda amewaasa Maafisa na Askari kuviishi viapo vyao wakati wote wanapotekeleza majukumu ya kijeshi.