Na Mwamvua Mwinyi, Pwani
Mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kufanya ziara ya kampeni mkoani Pwani, 28 Septemba mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Katibu wa Siasa, Uenezi na Mafunzo wa CCM Mkoa wa Pwani, David Mramba, alisema Dkt. Samia atahutubia mkutano mkubwa wa kampeni utakaofanyika katika viwanja vya Saba Saba, Kata ya Mkuza, Wilaya ya Kibaha.
Aidha, atafanya mikutano midogo ya kampeni katika maeneo ya Chalinze na Msata, Wilaya ya Bagamoyo.
“Lengo la mikutano hiyo ni kuwasilisha Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2025/2030, kuonyesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Awamu ya Sita, pamoja na kuwashukuru wananchi kwa kuendelea kukiamini Chama Cha Mapinduzi,” alibainisha Mramba.
Mramba aliwaomba wananchi wa Mkoa wa Pwani ,kujitokeza kwa wingi kushiriki mikutano hiyo ili wapate nafasi ya kumsikiliza mgombea wao, na hatimaye kujitokeza kwa wingi kumpigia kura tarehe 29 Oktoba mwaka huu, ili aendelee kuiongoza nchi.