Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma
Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora Jaji Mstaafu Mathew Mwaimu amesema kuwa Tume hiyo inatambua jitihada za Serikali na Wadau katika kuhakikisha Wanawake wanapata Haki zao na Kuwezeshwa kisiasa,kiuchumi na kijamii ambapo pamoja na jitihada hizo bado zipo changamoto kwao ikiwemo ukatili wa kijinsia na ushiriki mdogo katika shughuli za kiuchumi na kisiasa.
Ambapo Jaji Mstaafu Mwaimu ametoa mapendekezo ma nne kwa Serikali na Wadau ikiwemo kuendelea kuwezesha wanawake kiuchumi na kisiasa ili kuleta usawa katika jamii, pia Serikali na Wadau wengine kuendelea kutoa elimu itakayo wasaidia wanawake kutambua haki zao na kuzidai zinapovunjwa.
Jaji Mwaimu amesema hayo mapema Leo hii Jijini Dodoma Machi 7,2025 wakati akizungumza na Wanahabari akitoa Tamko la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) kuelekea Maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani machi 8,2025 yaliyobeba Kauli mbiu isemayo :”Wanawake Wasichana 2025: Tuimarishe Haki,Usawa na Uwezeshaji”
“THBUB inatambua jitihada mbalimbali za Serikali na wadau wengine katika kuhakikisha wanawake wanapata haki zao na kuwawezesha kisiasa,kiuchumi na kijamii. Lakini pamoja na jitihada hizo wanakabiliwa na changamoto zikiwemo vitendo vya ukatili wa kijinsia na uwezo mdogo wa kushiriki shughuli za kiuchumi na kisiasa”.
“Kutokana na changamoto hizo THBUB inapendekeza kuwa Serikali iendelee kuwawezesha wanawake kiuchumi na kisiasa ili kuleta usawa katika jamii,Serikali na wadau wengine waendelee kutoa elimu itakayo wasaidia wanawake kutambua haki zao nankuzidai zinapovunjwa,Jamii kuendelea kuzingatia sheria,haki haki za binadamu na misingi ya utawala bora ili kuleta usawa na wanawake wenyewe kuendelea kujiamini na kutumia fursa zilizopo kujiwezesha kiuchumi na kisiasa”.
Aidha amesema kuwa kauli mbiu ya mwaka huu inatukumbusha kuhusu wajibu wa jamii kuona umuhimu wa ujumuishi wa wanawake na wasichana katika mipango yote ya maendeleo,kusimama kidete kuhakikisha wanapata haki zao na fursa sawa katika nyanja zote za Maendeleo.
Na kuongeza kuwa kupitia Kaulimbiu hii jamii pia inapata fursa ya kujadili na kuandaa mikakati madhubuti itakayo saidia kutatua changamoto zinazowakabili wanawake, wasichana na makundi mengine yenye mahitaji maalum,zikiwemo zile zinazotokana na ukatili wa kijinsia ili kuleta usawa.
Umoja wa Mataifa uliridhia na kuanza kuadimisha rasmi siku ya Wanawake Duniani Machi 8 mwaka 1975 kwa lengo la kuikumbusha Dunia juu ya usawa wa kijinsia na Haki za Wanawake.