Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
MGODI wa Dhahabu wa Geita Gold Mining Limited (GGML) umetoa msaada wa pikipiki 15 kwa Jeshi la Polisi kwa lengo la kusaidia shughuli za doria na operesheni mbalimbali zinazolenga kuimarisha usalama wa raia na mali zao.
Akipokea Pikipiki hizo kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Camilius Wambura, Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Kamishna wa Polisi (CP) Awadhi Juma Haji amesema kuwa jeshi hilo linaushukuru mgodi huo kwa kuendelea kushirikiana na jeshi hilo katika kuimarisha ulinzi na usalama hapa nchini.
Amesema kuwa jukumu la ulinzi na usalama ni la kila mtu na jamii kwa ujumla, akiusifu mgodi huo kwa kuendelea kushirikiana na jeshi hilo na kusaidia maeneo mbalimbali ya maendeleo ya kijamii ikiwemo suala la ulinzi na usalama.
“Msaada huu utasaidia kuongeza ufanisi katika shughuli za kila siku za polisi, hususan katika maeneo yenye changamoto za miundombinu,”, amesema CP Awadhi.
Akikabidhi pikipiki hizo, Mshauri Mwandamizi wa masuala ya Kisheria kutoka Geita Gold Mine Ltd, David Nzaligo amesema kuwa mgodi huo unajivunia kuwa sehemu ya jamii kwa kutoa misaada mbalimbali pale inapohitajika.
Amesema usalama ni jukumu la kila mmoja kwa ajili ya maendeleo ya nchi na ndio maana wameamua kutoa msaada huo.
Viongozi mbalimbali wa jeshi hilo la polisi na maafisa wengine kutoka mgodi huo akiwemo Meneja Mwandamizi wa Usalama, Suleiman Machira walihudhuria makabidhiano hayo.