Na. Peter Haule na Saidina Msangi, Dodoma
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi na Utawala Bora, Mhe. George Simbachawene, ambaye ni mgeni rasmi katika ufunguzi rasmi wa Wiki ya Maadhimisho ya Utumishi wa Umma, ameipongeza Wizara ya Fedha na Taasisi zake kwa umahiri katika utoaji huduma alipotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Pongezi hizo amezitoa baada ya maelezo yaliyotolewa na Mkuu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Prof. William Pallangyo, kuhusu huduma zinazotolewa na Wizara kupitia Idara, Vitengo na Taasisi zake.
Prof. Pallangyo alizitaja huduma zinazotolewa katika Banda hilo kuwa ni pamoja na elimu kuhusu Elimu ya Fedha, Bajeti ya Serikali, Usimamizi wa Mali za Serikali, Pensheni ya Wastaafu inayotolewa na Hazina, Mifumo ya Fedha na Usimamizi wa Deni la Serikali.
Aliongeza kuwa huduma zinazotolewa na Taasisi za Wizara ya Fedha ni pamoja na Program zinazotolewa na Vyuo vilivyo chini ya Wizara lakini pia masuala ya Usimamizi wa Bima, Mifuko ya Uwekezaji na Takwimu rasmi.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Wizara ya Fedha, Bw. Lusius Mwenda, aliwataka watumishi wa Wizara ya Fedha, kuendelea kutoa huduma kwa Weledi katika kipindi chote cha maadhimisho hayo ili wananchi wapate uelewa wa masuala mbalimbali yanayotekelezwa na Wizara zikiwemo Sera na program za Wizara.
Wiki ya Maadhimisho ya Utumishi wa Umma imeanza Juni 16 na inatarajiwa kuhitimishwa Juni 23 mwaka huu ikiwa na kauli mbiu ya “Himiza Matumizi ya Mifumo ya Kidigiti ili kuongeza Upatikanaji wa Taarifa na Kuchangia Uwajibikaji”.








(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha)