MFANYABIASHARA, mdau wa maendeleo Kigamboni na Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), William Nyakua, leo amerejesha rasmi fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho ili kugombea nafasi ya Ubunge wa Jimbo la Kigamboni katika Uchaguzi Mkuu ujao wa Oktoba 2025.
Akizungumza baada ya kurejesha fomu hiyo, Nyakua amesema ameona ni wakati muafaka kuchukua jukumu la kuwatumikia wananchi wa Kigamboni kwa nafasi ya Ubunge ili kuendeleza juhudi za maendeleo zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Nimejipanga kuwaletea wananchi wa Kigamboni maendeleo ya kweli kupitia uongozi wa ushirikiano, uwazi na utekelezaji wa miradi yenye tija kwa jamii. Ninaamini katika nguvu ya umoja na kushirikiana na wananchi wote,” amesema Nyakua.
Hii ni hatua mojawapo ya mchakato wa ndani ya CCM wa kuwachuja na kuwateua wagombea watakaopeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu.