Na. Peter Haule na Joseph Mahumi,WF, Dar es Salaam
Baraza la Masoko ya Mitaji nchini Tanzania (CMT) limetafuta ufumbuzi wa migogoro ya umiliki na kucheleweshwa kwa malipo yanayotokana na masoko ya mitaji kwa wawekezaji na madalali.
Hayo yamebainishwa na Afisa Sheria na Utafiti wa Baraza hilo, Bw. Ademson Emmanuel wakati akitoa elimu kuhusu Baraza kwa wananchi waliotembelea Banda la Wizara ya Fedha katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Sabasaba) yanayoendelea katika Viwanja vya Sabasaba, Barabara ya Kilwa, jijini Dar es Salaam.
Alisema kuwa Baraza hilo ni Taasisi huru ya haki madai nchini linalotoa utatuzi wa migogoro ya masoko ya mitaji kwa haraka na haki kupitia kifungu cha 136A (1) ambapo hutatua migogoro baina ya wawekezaji, madalali, kampuni zilizoorodheshwa, mameneja wa mifuko ya uwekezaji na mamlaka za usimamizi.
“Endapo hukuridhishwa na maamuzi ya mamlaka ya usimamizi, mteja ana haki ya kukata rufaa kwa Baraza chini ya Kifungu cha 136H(1) ambapo Baraza linapitia maamuzi kwa umakini ili kuhakikisha yamezingatia sheria na usawa kwa lengo la kulinda haki na kuhimiza uwajibikaji kwenye sekta ya masoko na mitaji”, alisema Bw. Emmanuel.
Alisema kazi ya Baraza ni zaidi ya utatuzi wa migogoro, kwa kuwa linatoa tafsiri za Sheria za masoko ya mitaji kupitia Kifungu cha 136G (2) ambapo husaidia kuzuia mienendo isiyofaa na kuhakikisha masoko ya mitaji yanaendelea kuaminika.
Bw. Emmanuel alisema kuwa usalama wa wawekezaji ni sehemu ya msingi wa shughuli za Baraza ambapo usalama unaangazia eneo la uwekaji wa akiba au usimamizi wa mifuko ya kitaasisi kama UTT, alisema Baraza linachukua hatua madhubuti na za kuaminika dhidi ya ubadhirifu, utendaji mbovu na uvunjaji wa kanuni ili kulinda uwekezaji.
Mwenyekiti wa Baraza hilo ni Jaji wa Mahakama Kuu ambaye anahakikisha maamuzi yanayotolewa yanazingatia kanuni za kisheria na usawa, pia Baraza hilo lina wajumbe wanne ambao ni wataalamu wa fedha na sheria.




(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Fedha, Dar es Salaam)