Wakandarasi wa makampuni ya usafi jijini Dar es salaam wametakiwa kuhakikisha usalama wa wafanyakazi wao katika mazingira ya kazi zao.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya ya Ilala, Mkoani Dar es salaam, Edward Mpogolo, mara baada ya kukamilika kwa zoezi la usafi katika fukwe za bahari ya hindi.
Mpogolo amesema ni wakati wa wakandarasi kuwalinda wafanyakazi wao wanaofanya kazi za usafi barabarani kuwa na vifaa vinavyowawezesha kuwa salama kutoka kwa watumiaji wengine wa barabara hasa madereva wanaotumia vyombo vya moto usiku.
Akielezea juu ya mwamko wa taasisi na makampuni kuguswa katika kufanya usafi, Mpogolo amesema hiyo ni hatua kubwa kufikiwa katika halmashauri kwani zoezi la usafi ni la ushirikiano na kujitolea .
Aidha Mpogolo ametumia nafasi hiyo kumpongeza Mkurugenzi wa halmashauri ya jiji la Dar es salaam Elihuruma Mabelya, kwa kununua vifaa vya kufanyia usafi na kuongeza muda wa mikataba kwa wakandarasi hadi miaka mitatu tofauti ni mikataba ya awali iliyochukua muda mfupi.
Huku akiviomba vyombo vya habari kuendelea kupaza sauti kuelimisha wananchi juu ya ufanyaji usafi katika mazingira yao jambo litalosaidia kupunguza na kukabiliana na magonjwa ya mlipuko.
Mkuu huyo wa wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo, amebainisha pia sababu ya kufanya usafi wa mara kwa mara katika fukwe ni kutokana na tabia ya bahari kutupa uchafu nje hivyo usafi katika maeneo hayo utakua wa kudumu.
Kwa upande wa Mkurugenzi wa jiji la Dar es salaam Elihuruma Mabelya ameshukuru ushirikiano kutoka serikalini kwa utekelezaji zoezi la usafi kwao limekua na mafanikio kwa viongozi kuonyesha mfano wa kufanya usafi ili kujikinga na magonjwa.
Pamoja na kueleza maagizo yaliyotolewa na Mkuu wa wilaya, Edward Mpogolo juu ya mikataba ya wakandarasi, ununuzi wa vifaa vya kufanyia usafi na ushirikiano na wakandarasi katika uzoaji taka na ukusanyaji mapato yanaendelea kufanyiwa kazi.
Zoezi la usafi katika wilayani ilala, Mkoani Dar es salaam limeendelea kuwa la kudumu katika maeneo mbalimbali ya barabara, masoko na fukwe za bahari ya hindi.